BILIONI 37 ZATUMIKA UPANUZI WA UWANJA WA NDEGE SONGEA,RC AKAGUA NA KURIDHISHWA KAZI

Na Muhidin Amri,,Songea

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge,amekagua mradi wa upanuzi  na ukarabati wa uwanja wa ndege wa Songea na kuridhika na maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo.

Jenerali Ibuge amesema, matumaini ya Serikali ni kwamba mara kazi  itakapokamilika uwanja huo utaongeza  idadi kubwa ya abiria kwenda na kuja Songea,kwa kuwa hivi  baadhi ya wananchi wa mkoa jirani wa Njombe na Lindi wameanza kutumia uwanja wa  ndege Songea kwa safari mbalimbali hasa za kibiashara.

Ibuge amesema hayo, baada ya kukagua  uwanja huo unaofanyiwa upanuzi  kwa gharama ya Sh, bilioni 37  kazi inayotekelezwa na Kampuni ya Chico ya China na Wakala wa Barabara(Tanroad)mkoa wa Ruvuma.

Amesema, tangu upanuzi wa uwanja ulipoanza kumewezesha  kuongeza safari za ndege kutoka mbili za awali hadi tatu kwa wiki na  kuishukuru serikali kwa kutoa fedha zilizowezesha kazi ya  upanuzi kufanyika kwa ufanikisi makubwa.

“baada ya upanuzi unaondelea kufanyika safari za ndege zinafanyika siku ya Jumatatu,Jumatano na Ijumaa  kupitia Shirika la Ndege Tanzania ATCL,uwanja  uko salama na sisi wana Kusini hususani wakazi wa mkoa wa Ruvuma  tunataka kufikisha biashara zetu kwa haraka  zifike mikoa mingine hapa nchini”amesema.

Aidha, ameishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kutokana na dhamira ya kuboresha miundombinu  ya usafiri ikiwemo uwanja wa ndege na Barabara zinazoendelea kujengwa katika mkoa wa Ruvuma.

Ametoa Rai kwa wananchi wa Ruvuma na wale kutoka mikoa jirani ya Nyanda za juu kusini,kutumia uwanja huo kwa ajili ya kusafiri na kurahisisha safari kutoka Songea kwenda maeneo mbalimbali ya nchi yetu kwani uwanja huo uko tayari.

Pia amesema, kufungua kwa uwanja huo kutasaidia kupanua wigo wa nafasi ya utalii katika mkoa huo ambao  umebarikiwa kuwa na vivutio vingi vya utalii.

Ibuge amevitaja vivutio hivyo ni pamoja na fukwe za Ziwa Nyasa, safu za milima ya Matogoro,Milima ya Livingstone,Hifadhi ya Taifa ya Nyerere,Makumbusho ya Mashujaa wa Vita ya Majimaji na Pori la la Liparamba.

Kwa upande wake Meneja wa Tanroad mkoa wa Ruvuma Razak Alilanuswe amesema,uwanja wa  ndege wa Songea unajengwa kwa gharama ya Sh.bilioni 37.09 ambapo kazi zilikamilika hadi sasa ni sehemu ya kuruka na kutua ndege,kuchora mistari.

Kwa mujibu wa Razak, kazi zilizobaki ni mnara wa kuongozea Ndege, na  kufunga taa ambapo kwa sasa uwanja huo utakuwa na urefu wa mita 1,860  kutoka mita 1,600 za awali,hivyo kukidhi vigezo vya kutua ndege aina yeyote na wakati wowote.

Meneja wa Uwanja huo Jordan Mchami amesema, baada ya upanuzi na ukarabati wa uwanja huo idadi ya abiri wanaotumia  usafiri wa ndege imeongezeka kutoka 17 hadi 70.

Amesema, awali ndege iliyokuwa inatuja ni ndugo  yenye uwezo wa kubeba abiria 13 tu  na nauli ya safari moja  ilikuwa Sh.  600,000 na kwenda na kurudi gharama ilikuwa Sh.1,000,000.

Amesema,kutokana na upanuzi unaoendelea  na kuanza kwa safari za ndege kwa kutumia ndege za ATCL nauli imeshuka hadi kufikia Sh. 250,000 kwa safari moja ambapo kwenda na kurudi ni Sh.375,000.



source https://fullshangweblog.co.tz/2021/10/19/bilioni-37-zatumika-upanuzi-wa-uwanja-wa-ndege-songearc-akagua-na-kuridhishwa-kazi/

0 Comments

banner

Ahsante kwa kutembelea zotekali blog ili kuwa karibu nasi kila wakati Jiunge katika kurasa zetu zamitandao ya kijamii  facebook , Twitter, Instagram na Youtube  NI BUREE